Kiswahili

Radoje Domanović (Februari 16, 1873 – Agosti 17, 1908) alikuwa mwandishi wa Serbia, mwandishi wa habari na mwalimu, maarufu sana kwa hadithi fupi za kejeli.

Radoje Domanović alizaliwa katika kijiji cha Ovsište huko Serbia ya Kati, mtoto wa mwalimu wa mtaa na mjasiliamali Miloš Domanović, na Persida Cukić, ukoo wa Pavle Cukić, mmoja wa makamanda wa jeshi la Mapinduzi ya Serbia ya Kwanza na ya Pili. Alitumia utoto wake katika kijiji cha Gornje Jarušice karibu na Kragujevac, ambapo alienda shule ya msingi. Alihitimu shule ya kati huko Kragujevac, na Kitivo cha Falsafa katika Chuo Kikuu cha Belgrade, ambapo alisoma lugha ya Serbia na historia.

Mnamo 1895, Domanović aliteuliwa kwa mara kwanza, kazi ya kufundisha huko Pirot, kusini mwa Serbia, mkoa ambao uliokolewa hivi karibuni kutoka kwa Dola ya Ottoman. Huko Pirot, alikutana na Jaša Prodanović (1867–1948), mwalimu na mwanaharakati ambaye alisaidia kuunda maoni yake ya kisiasa. Huko pia alikutana na mkewe wa siku zijazo, Natalija Raketić (1875–1939), mwalimu masikini wa shule kutoka Sremski Karlovci, ambaye atamuunga mkono katika maisha yake mafupi na yenye misukosuko, na ambaye alipata nae watoto watatu.

Tangu alipojiunga na Chama cha Upinzani cha People’s Radical, alipata msuguano na Utawala wa nasaba wa Obrenović, na alihamishiwa Vranje mwishoni mwa 1895, na kisha mnamo 1896 akahamishwa tena kwenda Leskovac. Kazi ya uandishi ya Domanović pia ilianza wakati wa siku zake za kufundisha, alipochapisha hadithi fupi ya ukweli mnamo 1895. Baada ya kuonekana kwake kwa kwanza mbele ya umma akiipinga serikali mnamo 1898, yeye na mkewe walifukuzwa kazi ya umma, na Domanović alihama na familia yake kwenda Belgrade.

Huko Belgrade alianza kufanya kazi na waandishi wenzake katika “Zvezda” (Nyota) jarida la kila wiki na gazeti la kisiasa la upinzani “Odjek” (Mwangwi). Kwa wakati huu alianza kuandika na kuchapisha hadithi zake za kejeli, kama “Pepo” na “Kukomesha kwa tamaa”. Kuibuka kwa umaarufu wa Radoje kulikuja na uchapishaji wa hadithi zake maarufu, “Kiongozi” (1901) na “Stradija” (1902), ambapo alishambulia kwa uwazi na kuweka wazi unafiki na udanganyifu wa utawala.

Baada ya mapinduzi ambayo yalimaliza kutawala kwa Aleksandar Obrenović mnamo 1903, kwenye kilele cha umaarufu wake, Domanović alipokea barua ya mwandishi katika Wizara ya Elimu, na serikali mpya ilimpa idhini kwenda Ujerumani kwa mwaka mmoja wa ubobezi, ambao aliutumia huko Munich. Kurudi huko Serbia, Radoje alijikuta akikatishwa tamaa na ukosefu wa mabadiliko yoyote ya kweli katika jamii. Alianzisha jarida lake mwenyewe la wiki la kisiasa, “Stradija”, ambalo aliendelea kukosoa udhaifu wa demokrasia mpya, lakini uandishi wake haukuwa na nguvu na msukumo ambao ulikuwa nao awali.

Radoje Domanović alikufa nusu saa baada ya usiku wa manane mnamo Agosti 17, 1908, akiwa na umri wa miaka 35, baada ya mapigano marefu na nimonia sugu na kifua kikuu. Alizikwa kwenye makaburi mapya ya Belgrade. Kazi zake zilizobaki ambazo hazikuchapishwa zilipotea wakati wa Vita Vya Dunia I.

Kazi ya fasihi

Baadhi ya kazi maarufu zaidi za Radoje Domanović ni pamoja na:

  • Bahari iliyokufa, 1902
  • Chapa, 1899
  • Hoja ya ng’ombe wa kawaida wa Serbia, 1902
  • Kiongozi, 1901
  • Kukomesha kwa tamaa, 1899
  • Kraljević Marko kati ya Waserbia kwa mara ya pili, 1901
  • Pepo, 1898
  • Stradija, 1902
  • Uasi wa kisasa, 1902

Mradi wa “Radoje Domanović” upo kwenye uangalizi wa Vladimir Živanović, mhandisi wa ubora na msomaji wa fasihi, kwa lengo la kuorodhesha kazi kamili za mwandishi wa Serbia Radoje Domanović kidijitali, na kuwezesha wasomaji kutoka ulimwenguni kote kusoma kazi za asili na tafsiri zake. Hadithi zifuatazo zilitafsiriwa haswa kwa Mradi, na zimechapishwa hapa kwa mara ya kwanza:

Kwa Mradi wa “Radoje Domanović” uliotafsiriwa na John N. Lusingu mnamo Mei 2020.

 

 


[Contents of this biographical reference page were written for the “Radoje Domanović” Project with the goal of promoting the life and works of the famous Serbian satirist, Radoje Domanović, and are released into public domain. Editor]

%d bloggers like this: