Tag Archive | ushujaa

Kiongozi (3/3)

(ukurasa uliopita)

Kama hivyo siku ya kwanza ilipita, na ikifuatiwa na siku zaidi na mafanikio kama yale. Hakuna kitu cha umuhimu mkubwa sana kilitokea, matukio ya kawaida tu: walidondoka kutanguliza vichwa kwenye shimo, kisha ndani ya bonde; walikwanguliwa kwenye visiki na kwenye vichaka vya forosadi nyeusi; walikanyaga chupa; kadhaa walivunjika mikono na miguu; wengine waliugua pigo kichwani. Lakini mateso haya yote yalivumiliwa. Wazee wachache waliachwa wamekufa kando ya barabara. “Wangekufa tu hata wangekuwa wamekaa nyumbani, bila kuja barabarani!” wasemaji walisema, wakiwatia moyo wengine kuendelea. Watoto wadogo wachache, mwaka mmoja hadi miaka miwili, pia waliangamia. Wazazi walishikiilia maumivu ya mioyo yao kwa sababu ilikuwa mapenzi ya Mungu. “Na kwa watoto wadogo zaidi, ndivyo ambavyo huzuni ilikua ndogo. Wakati wanapokuwa wachanga zaidi huzuni ni ndogo. Mungu awasaidie wazazi wasipoteze watoto wao wakati wamefikia umri wa kuoa. Ikiwa watoto wamepania sana, ni bora wafe mapema. Halafu huzuni sio kubwa sana!” wasemaji waliwatia moyo tena. Baadhi yao walifunga vitambaa kichwani na kuweka vibonyezo vya baridi kwenye michubuko yao. Wengine walibeba mikono yao kwenye vitambaa na kuining’iniza. Wote walikua wamechakaa na kukatwa. Nguo zao zilining’inia kwa michano, lakini walisonga mbele kwa furaha. Hii yote ingekuwa rahisi kuvumilia ikiwa hawakuwa wamejawa na njaa mara nyingi. Lakini ilibidi waendelee.

Siku moja, kitu muhimu kilitokea.

Kiongozi alikuwa anatembea mbele, akizungukwa na wanaume jasiri zaidi katika kundi hilo. (Wawili kati yao walikosekana, na hakuna mtu aliyejua walikuwa wapi. Ilikuwa wazi kwa wote kwamba walikuwa wamesaliti dhumuni lao na wakakimbia. Katika hafla moja msemaji alisema kitu juu ya uasi wao wa aibu. Ni wachache tu waliamini wawili hao walikuwa wamekufa njiani, lakini hawakutoa maoni yao ili wasiwashawishi wengine.) Kikundi kilichobaki kilikuwa nyuma yao. Ghafla lilionekana bonde kubwa sana na kina, kina kirefu sana hakika. Mteremko ulikuwa mkali sana kiasi kwamba hawakuthubutu kuchukua hatua moja mbele. Hata wenye ujasiri sana walisimama ghafla na kumtazama kiongozi. Akiwa amenuna, na kutekwa na mawazo kichwa chake kikiwa chini, akasogea mbele kwa ujasiri, akagonga fimbo yake mbele, kwanza kulia, kisha kushoto, kama kawaida yake. Wengi walisema haya yalimfanya aonekane mwenye heshima zaidi. Hakuangalia mtu yeyote wala kusema chochote. Kwenye uso wake hakukuwa na mabadiliko yoyote wala ishara ya hofu wakati yeye anakaribia karibu na eneo hili tupu. Hata wanaume wenye ujasiri zaidi wakawa kama kifo, lakini hakuna mtu aliyethubutu kumuonya kiongozi shujaa, mwenye busara. Hatua mbili zaidi na alikuwa ukingoni. Kwa hofu kali na kwa macho kodo, wote walitetemeka. Wanaume wenye ujasiri walikuwa katika hatua ya kumrudisha kiongozi nyuma, hata ikiwa ilimaanisha kukiuka kwa nidhamu, wakati alipokanyaga mara moja, mara mbili, na kutumbukia kwenye bonde. Kukatokea mshangao, kuomboleza, kupiga mayowe; hofu ikatawala. Wengine walianza kukimbia.

– Subiri, ndugu! Je! Haraka ya nini? Je! Hivi ndivyo unavyotunza ahadi yako? Lazima tumfuate mtu huyu mwenye busara kwa sababu anajua anachokifanya. Angekuwa mwendawazimu kujiangamiza. Mbele, tumfuate! Hii ndio hatari kubwa na labda ya mwisho, shida ya mwisho. Nani anajua? Labda kwa upande mwingine wa bonde hili tutapata ardhi ya kutosha, yenye rutuba ambayo Mungu alituwekea sisi. Mbele! Bila kujitolea, hatutafika popote! – hayo yalikuwa maneno ya ushauri ya msemaji na yeye pia alichukua hatua mbili mbele, na kutoweka kwenye bonde. Jasiri zaidi walifuata na kisha kila mtu akaingia.

Kulikuwa na kuomboleza, kuugulia, kugongana, kulia kwenye mteremko wa mwinuko huu mkubwa. Mtu angekuwa akiapa kwamba hakuna mtu atakayetoka akiwa hai, bila kuumia vibaya na awe na mwili mmoja, lakini maisha ya mwanadamu ni magumu. Kiongozi alikuwa na bahati isiyo ya kawaida. Alining’inia kwenye kichaka wakati anaanguka hivyo hakuumia. Aliweza kujiondoa pamoja na kushuka. Wakati kelele, kuomboleza na kulia kumejaa chini, alikaa bila kusogea, kimya kabisa. Wachache ambao walipigwa kwa hasira walianza kumtukana lakini hakujali. Wale ambao kwa bahati nzuri waliweza kushikilia kichaka au mti wakati wa kuanguka walianza kujaribu kushuka. Wengine walikuwa wamevunjika vichwa hivyo kwamba damu ilikuwa ikiwatoka usoni mwao. Hakukuwa na mtu mwenye amani isipokuwa kiongozi. Wote walimkasirikia na kuugulia uchungu lakini hata hakuinua kichwa chake. Alikuwa kimya na kubaki kwenye mkao wa mtu mwenye busara!

Wakati ulipita. Idadi ya wasafiri ilikuwa inakuwa ndogo na ndogo. Kila siku ilichukua chake. Wengine waliacha kikundi na kurudi nyuma.

Kati ya idadi kubwa iliyoanza, ni karibu ishirini tu waliobaki. Nyuso zao, zilizochoka zilionyesha ishara za kukata tamaa, shaka, uchovu na njaa, lakini hakuna mtu alisema neno. Walikuwa kimya kama kiongozi wao na waliendelea kujivuta pamoja. Hata msemaji mwenye roho alitikisa kichwa kwa matamanio. Barabara ilikuwa ngumu kweli.

Idadi yao ilipungua kila siku hadi ikafikia kumi tu. Kwa sura zenye huzuni, waliugua na kulalamika badala ya kuongea.

Walionekana kama vilema kuliko wanaume. Wengine walikuwa kwenye magongo ya kutembelea. Wengine walishikilia mikono yao kwa vitambaa vilivyofungwa shingoni mwao. Juu ya mikono yao kulikuwa na bandeji nyingi na vigandamizio. Hata kama wangetaka kujitoa upya, hawangeweza kwa sababu miili yao haikua na nafasi ya majeraha yoyote mapya.

Hata wenye nguvu na jasiri zaidi kati yao walikuwa wameshapoteza imani na tumaini lakini bado walipambana zaidi; hivyo, walitapatapa namna fulani kwa bidii kubwa, wakilalamika, wamejaa maumivu. Nini kingine wangeweza kufanya ikiwa hawawezi kurudi nyuma? Sadaka nyingi na sasa kuachana na safari?

Kisukusuku kilishuka. Wakichechemea kwenye magongo ya kutembelea, ghafla waliona kwamba kiongozi huyo hakuwa mbele yao tena. Hatua nyingine na wote wameingia kwenye bonde lingine.

– Ah, mguu wangu! Oo, mkono wangu! – sauti zililia na kuugulia. Sauti moja dhaifu ilimlaani kiongozi anayestahili kisha alikaa kimya.

Jua lilipochomoza, hapo alikaa kiongozi, sawa na siku ile alipochaguliwa. Hakukuwa na mabadiliko yoyote  kabisa katika muonekano wake.

Msemaji akapanda nje ya bonde, akifuatiwa na wengine wawili. Wakiwa wamechakaa na wenye damu, waligeuka kuona ni wangapi wamebaki, kumbe walibaki wao tu. Hofu ya dhati na kutokuwa na tumaini vilijaza mioyo yao. Kanda hiyo haikujulikana, milima, miamba – hakuna njia mahali popote. Siku mbili kabla hawajafika barabarani lakini waliiacha nyuma. Kiongozi aliwaongoza huko.

Walifikiria juu ya marafiki na jamaa wengi ambao walikuwa wamekufa kwenye safari hii nzuri. Huzuni iliyo na nguvu kuliko maumivu kwenye miguu yao yenye ulemavu iliwashinda. Walikuwa wameshuhudia uharibifu wao wenyewe kwa macho yao wenyewe.

Msemaji akapanda kwa kiongozi huyo na kuanza kuongea kwa sauti iliyochoka, inayotetemeka iliyojaa maumivu, kukata tamaa na uchungu.

– Je! Tunakwenda wapi sasa?

Kiongozi alikuwa kimya.

– Unatupeleka wapi na umetuleta wapi? Tulijiweka sisi na familia zetu mikononi mwako na tukakufuata, tukiziacha nyumba zetu na kaburi za mababu zetu kwa matumaini kwamba tunaweza kujiokoa na dhiki katika nchi hiyo tasa. Lakini umetuharibu kwa njia mbaya zaidi. Kulikuwa na familia mia mbili nyuma yako na sasa tazama ni wangapi!

– Unamaanisha kila mtu hayuko hapa? – alinong’oneza kiongozi bila kuinua kichwa chake.

– Unawezaje kuuliza swali kama hilo? Angalia juu uone! Hesabu ni wangapi wetu tumebaki kwenye safari hii mbaya! Angalia hali ya miili yetu ilivyo! Itakuwa afadhali kufa kuliko kuwa kilema namna hii.

– Siwezi kukutazama!

– Kwa nini isiwe hivyo?

– Mimi ni kipofu.

Kimya kikatawala.

– Je! Umepoteza mtazamo wako wakati wa safari?

– Nilizaliwa kipofu!

Watatu hao waliinamisha vichwa vyao kwa kukata tamaa.

Upepo wa vuli ulipuliza vibaya kupitia milimani na kupuputisha majani yaliyokauka. Ukungu ulizunguka juu ya vilima, na kupitia baridi, ya hewa yenye unyevu ilipeperusha manyoya ya kunguru. Ndege wa mkosi alilia. Jua lilikuwa limefunikwa nyuma ya mawingu, ambayo yalikuwa yakijizungusha mbali zaidi na zaidi.

Watatu waliangaliana kila mmoja kwa mshtuko mkubwa.

– Je! Tunaweza kwenda wapi sasa?

– Hatujui!

 

Huko Belgrade, 1901
Kwa mradi wa “Radoje Domanović” uliotafsiriwa na John N. Lusingu, 2020

Chapa

Nilikuwa na ndoto mbaya. Sishangai sana kuhusu ndoto yenyewe, lakini ninashangaa ni jinsi gani ningeweza kupata ujasiri wa kuota mambo mabaya, wakati mimi ni raia mtulivu na mwenye heshima mwenyewe, mtoto mtiifu wa mama yetu mpendwa, anayeteseka Serbia, kama watoto wake wengine wote. Kwa kweli, unajua, kama ningekuwa wa kipekee katika kitu chochote, itakuwa tofauti, lakini hapana, rafiki yangu mpendwa, mimi hufanya sawa sawa kabisa na watu wengine, na kwa kuwa mwangalifu katika kila kitu, hakuna mtu anayeweza kulinganishwa nami hapo. Wakati mmoja niliona kitufe cha rangi ya sare ya polisi kikiwa kimekaa barabarani, na nikatazama mng’ao wake wa miujiza, karibu naelekea kupita, nikiwa nimejawa na kumbukumbu nzuri, wakati ghafla, mkono wangu ukaanza kutetemeka na ukachomoka na kupiga saluti; kichwa changu kiliinamia ardhi yenyewe, na mdomo wangu ukaenea ndani ya tabasamu hilo zuri ambalo sisi sote tulilivaa tunapowasalimu wakuu wetu.

– Damu tukufu inapita kwenye mishipa yangu – ndivyo ilivyo! – Hichi ndicho nilifikiria wakati huo na nilitazama kwa dharau watu wakatili waliopita na kukikanyaga kifungo kile bila kujali.

– Mkatili! – Nilisema kwa uchungu, nikatema mate, kisha nikaondoka kimya kimya, nikiwa nimefarijiwa na wazo kwamba wakatili kama hao ni wachache; na nilifurahi sana kuwa Mungu alikuwa amenipa moyo uliosafishwa na utukufu, damu karimu ya babu zetu.

Kweli, unaweza kuona sasa mimi ni mtu mzuri sana, sio tofauti kabisa na raia wengine wenye heshima, na bila shaka utashangaa jinsi mambo mabaya na ya kipumbavu yanaweza kutokea katika ndoto zangu.

Hakuna kitu kisicho cha kawaida kilinitokea siku hiyo. Nilikula chakula cha jioni kizuri na baadaye nikakaa kuchokonoa meno yangu kwa starehe; nikinywa divai yangu, kisha, baada ya kutumia haki yangu ya kishujaa na kizalendo kama raia, nilienda kitandani na nikachukua kitabu ili niweze kulala haraka zaidi.

Kitabu hicho kilianguka haraka kutoka kwenye mikono yangu, ambapo, kwa kweli, kiliridhisha hamu yangu na, majukumu yangu yote kukamilika, nikalala bila hatia kama mwana-kondoo.

Ghafla nilijikuta kwenye barabara nyembamba, yenye matope iliyoelekea kwenye milima. Usiku wenye baridi na mweusi. Upepo ulipuliza kati ya matawi tasa na kukata kama wembe kila unapogusa ngozi. Anga nyeusi, bubu, na ya kutisha, na theluji, kama mavumbi, ikipuliza macho ya mtu na kupiga juu ya uso. Hamna roho iliyo hai popote. Nina haraka na mara kwa mara nateleza kwenye barabara yenye matope kuelekea mara kushoto, mara kulia. Ninatetemeka na kuanguka na mwishowe nikapoteza njia, naendelea kutembea – Mungu anajua wapi – na sio usiku mfupi, wala wa kawaida, lakini kwa muda mrefu kama karne, na ninatembea wakati wote bila kujua ni wapi.

Hivyo nilitembea kwa miaka mingi sana na nilifika mahali, mbali, mbali na nchi yangu ya asili kwenda sehemu isiyojulikana ya ulimwengu, kwenda nchi ya kushangaza ambayo labda hakuna mtu anaijua na ambayo, nina hakika, inaweza kuonekana tu kwenye ndoto.

Kuzurura ardhini pale nilifika katika mji mkubwa ambao watu wengi walikuwa wakiishi. Katika soko kubwa la watu kulikuwa na umati mkubwa, kelele nyingi ikiendelea, ya kutosha kupasua ngoma ya sikio la mtu. Niliingia kwenye mgahawa uliyoangaliana soko na nikamuuliza mwenye nyumba kwanini watu wengi wamekusanyika pamoja…

– Sisi ni watu watulivu na wenye heshima, – alianza simulizi yake, – sisi ni waaminifu na watiifu kwa Chifu.

– Chifu sio mamlaka ya juu kabisa? – Niliuliza, nikimkatiza.

– Chifu anatawala hapa na yeye ndiye mamlaka ya juu; kisha polisi wanafuatia.

Nilicheka.

– Kwanini unacheka?… Je! Hukujua?… Unatoka wapi?

Nilimwambia jinsi nilivyopotea, na kwamba nimetoka nchi ya mbali – Serbia.

– Nimesikia kuhusu nchi hiyo maarufu! – alimnong’oneza mwenye nyumba mwenyewe, akiniangalia kwa heshima, kisha akasema kwa sauti:

– Hiyo ndio njia yetu, – aliendelea, – Chifu anatawala hapa na polisi wake.

– Je! Polisi ni wa aina gani?

– Kweli, kuna aina tofauti za polisi – hutofautiana, kulingana na vyeo vyao. Kuna wanaojitambua na wasiojitambua… Sisi ni, unajua, watu tulivu na wenye heshima, lakini kila aina ya wazururaji hutoka kwa majirani, watufisadi na kutufundisha mambo mabaya. Ili kutofautisha kila raia wetu na watu wengine Chifu alitoa agizo jana kwamba raia wetu wote waende katika Korti ya mtaa, ambapo kila mmoja wetu atapewa na chapa kwenye paji la uso wake. Hii ndio sababu watu wengi wameungana: ili kushauriana nini cha kufanya.

Nilishtuka na kudhani kwamba napaswa kukimbia kutoka nchi hii ya kushangaza haraka iwezekanavyo, kwa sababu mimi, ingawa natokea Serbia, sikuweza kutumiwa kuonyesha moyo ya chivalry, na nilikuwa na wasiwasi kidogo juu yake!

Mmiliki wa nyumba alicheka kwa ukarimu, akanigonga begani, akasema kwa ukarimu:

– Ah, mgeni, hii inatosha kukutia woga? Haishangazi, lazima uende mbali ili kupata ujasiri kama wetu!

– Na unamaanisha kufanya nini? – Niliuliza kwa hofu.

– Ni swali gani! Utaona jinsi gani sisi ni jasiri. Lazima uende mbali zaidi ili upate ujasiri kama wetu, nakwambia. Umesafiri mbali sana na kuuona ulimwengu, lakini nina uhakika haujawahi kuona mashujaa wakubwa kuliko sisi. Wacha tuende huko pamoja. Lazima niharakishe.

Tulikuwa tu karibu kwenda wakati tuliposikia, mbele ya mlango, sauti wa mjeledi.

Nikachungulia nje: kulikuwa na kitu cha kuangalia – mtu mwenye taji yenye kung’aa, yenye pembe tatu kichwani mwake, amevaa suti angavu sana, alikuwa amepanda mgongo wa mtu mwingine akiwa amevaa nguo tajiri za kawaida, za raia. Alisimama mbele ya mgahawa na yule mpandaji akashuka.

Mmiliki wa nyumba akatoka, akainama chini, na yule mtu aliyevaa suti ya gaudy akaenda ndani ya mgahawa kwenye meza iliyopambwa sana. Yule katika nguo za raia alikaa mbele ya mgahawa na akasubiri. Mmiliki wa nyumba alimsujudia pia.

– Je! Yote haya ni nini? – Nilimuuliza mwenye nyumba, huku nimeshangazwa sana.

– Kweli, yule aliyeingia ndani ya mgahawa ni polisi wa hali cheo cha juu, na mtu huyu ni mmoja wa raia wetu mashuhuri, tajiri sana, na mzalendo mkubwa, – alinong’ona mwenye nyumba.

– Lakini kwa nini anamruhusu yule mwingine ampande mgongoni?

Mwenye nyumba akatikisa kichwa chake na tukasogea pembeni. Alinipa tabasamu la kudharau na kusema:

– Tunachukulia ni heshima kubwa na ya nadra! – Aliniambia vitu vingi sana ila, lakini nilifurahi sana kwa kuwa sikuweza kuvielewa. Lakini nilisikia wazi kabisa alichosema mwishoni: – Ni huduma kwa nchi ya mtu ambayo mataifa yote bado hayajajifunza kuthamini!

Tulifika kwenye mkutano na uchaguzi wa mwenyekiti ulikuwa tayari unaendelea.

Kundi la kwanza liliweka mtu anayeitwa Kolb, ikiwa nakumbuka jina sawasawa, kama mgombea wake wa kiti; kundi la pili lilimtaka Talb, na la tatu lilikuwa na mgombea wao wenyewe.

Kulikuwa na wasiwasi wa kutisha; kila kundi lilitaka kushinikiza mtu wake mwenyewe.

– Nadhani hatuna mtu bora kuliko Kolb kuwa mwenyekiti wa mkutano muhimu kama huu, – ilisema sauti kutoka kwa kundi la kwanza, – kwa sababu sote tunajua vyema sifa zake kama raia na ujasiri wake mkubwa. Sidhani kama kuna mtu yeyote kati yetu hapa anayeweza kujivunia kwa kuwa amekuwa akiendeshwa mara kwa mara na watu muhimu sana…

– Wewe ni nani kuongea juu yake, – alimtuliza mtu kutoka kikundi cha pili. – Haujawahi kupakiwa na karani wa polisi wa mdogo!

– Tunajua fadhila zako ni zipi, – alilia mtu kutoka kundi la tatu. – Kamwe hauwezi kupata pigo moja la mjeledi bila kuomboleza!

– Wacha tuelewane hili, ndugu! – alianza Kolb. – Ni kweli kwamba watu mashuhuri walikuwa wakipanda mgongoni mwangu mapema tangu miaka kumi iliyopita; walinipiga viboko na sikuwahi kutoa kilio, lakini inaweza kuwa kuna wanaostahili zaidi kati yetu. Labda kuna wadogo walio bora zaidi.

– Hapana, hapana, – walilia wafuasi wake.

– Hatutaki kusikia kuhusu heshima zilizopitwa na wakati! Ni miaka kumi tangu Kolb alipokuwa amepandwa mgongoni, – wakakemea kutoka kundi la pili.

– Damu changa inachukua hatamu, acheni mbwa mzee watafune mifupa ya zamani, – akaita mwengine kutoka kundi la tatu.

Ghafla hakukuwa na kelele tena; watu walisogea nyuma, kushoto na kulia, kusafisha njia na nikaona kijana mdogo wa karibu miaka thelathini. Alipokaribia, vichwa vyote viliinama.

– Huyu ni nani? – Nilimnong’oneza mwenye nyumba yangu.

– Yeye ndiye kiongozi maarufu. Kijana, lakini mwenye matumaini sana. Katika siku zake za awali aliweza kutamba kuwa alimbeba Chifu mgongoni mwake mara tatu. Yeye ni maarufu kuliko mtu yeyote.

– Labda watamchagua? – Niliuliza.

– Hiyo ni zaidi ya hakika, kwa sababu kwa wagombea wengine wote – wote ni wazee, wakati umewapita, wakati Chifu alipanda kwa muda kidogo nyuma ya mgongo wake jana.

– Jina lake ni nani?

– Kleard.

Walimpa mahali pa heshima.

– Nadhani, – sauti ya Kolb ilivunja ukimya, – kwamba hatuwezi kupata mtu bora kwa nafasi hii kuliko Kleard. Yeye ni mchanga, lakini hakuna hata mmoja wetu wazee ni sawa naye.

– Sikiliza, sikiliza!… Maisha marefu Kleard!… – sauti zote zilinguruma.

Kolb na Talb walimpeleka mahali pa mwenyekiti. Kila mtu alimwinamia kwa kina, na kulikuwa na ukimya kabisa.

– Asanteni, ndugu, kwa shukrani zenu za juu na heshima hii mmenipa kwa makubaliano. Matumaini yenu, ambayo yapo kwangu sasa, ni ya kufurahisha. Sio rahisi kuendesha matakwa ya taifa kupitia siku hizi ngumu, lakini nitafanya kila kitu kwa nguvu zangu kuhalalisha uaminifu wenu, kuwakilisha maoni yenu kwa uaminifu, na kustahili kuthaminiwa kwa hali ya juu kutoka kwenu. Asante, ndugu zangu, kwa kunichagua.

– Oyee! Oyee! Oyee! – Wapiga kura walitetemesha kutoka pande zote.

– Na sasa, ndugu, nina imani mtaniruhusu kusema maneno machache juu ya tukio hili muhimu. Si rahisi kuteseka kwa maumivu kama haya, mateso kama haya ambayo yamehifadhiwa kwa ajili yetu; si rahisi paji la uso na mtu kuwekwa chapa kwa chuma cha moto. Kwa kweli, hapana – ni uchungu ambao sio watu wote wanaweza kuvumilia. Wacha waoga watetemeke, waache watetemeke kwa woga, lakini hatupaswi kusahau hata kwa muda mfupi kwamba sisi ni wana wa mababu jasiri, damu tukufu inatembea kwenye mishipa yetu, damu ya kishujaa ya babu zetu, mashujaa wakuu ambao walikufa bila kufunga kope kwa uhuru na kwa faida yetu sisi wote, na kizazi chao. Mateso yetu ni kidogo, ikiwa utafikiria kuhusu mateso yao – je! Tuishi kama washiriki wa uzao mbaya na waoga kwa kuwa tunaishi vizuri zaidi kuliko hapo zamani? Kila mwenye uzalendo wa kweli, kila mtu ambaye hataki kuweka aibu taifa letu mbele ya ulimwengu wote, atabeba uchungu kama mwanaume na shujaa.

– Sikiliza! Sikiliza! Maisha marefu Kleard!

Kulikuwa na wasemaji kadhaa wenye bidii baada ya Kleard; waliwatia moyo watu waliogopa na kurudia zaidi au kidogo ya yale Kleard aliyoyasema.

Ndipo mzee aliyechoka, mwenye uso uliojikunja, nywele zake na ndevu nyeupe kama theluji, aliomba kusema. Magoti yake yalikuwa yametetemeka kwa uzee, mikono yake ilikuwa ikitetemeka, mgongo wake ukiwa umeinama. Sauti yake yenye mawimbi, macho yake yalikuwa angavu kwa machozi.

– Watoto, – alianza, machozi yakimtiririka kwenye mashavu yake na kudondokea kwenye ndevu zake nyeupe, – Nina huzuni na nitakufa hivi karibuni, lakini kwangu mimi niliona afadhali usikubali aibu kama hiyo ije kwenu. Nina umri wa miaka mia moja, na nimeishi maisha yangu yote bila hiyo!… Je! Kwa nini chapa ya utumwa ipandikizwe juu ya kichwa changu nyeupe na dhaifu sasa?…

– Chini kwa kizee! – mwenyekiti akapiga kelele.

– Chini naye! – wengine walipiga kelele.

– Mzee mwoga!

– Badala ya kutia moyo vijana, anatia hofu kila mtu!

– Anapaswa kuonea aibu nywele zake za kijivu! Ameishi muda mrefu wa kutosha, na bado anaweza kuogopa – sisi ambao ni vijana ni hodari zaidi…

– Chini na mwoga!

– Mtupe nje!

– Chini naye!

Umati wa watu jasiri na wenye hasira, vijana wazalendo walimkimbilia yule mzee na kuanza kumsukuma, kuvuta, na kumpiga kwa ukali wao.

Mwishowe walimwacha aende kwa sababu ya uzee wake – vinginevyo wangekuwa wamempiga mawe akiwa hai.

Wote waliapa kuwa jasiri kesho na kujionyesha wanastahili heshima na utukufu wa taifa lao.

Watu waliondoka kwenye mkutano kwa utaratibu mzuri. Waliokuwa wanajitenga walisema:

– Kesho tutaona nani ni nani!

– Tutawachambua wanaojivuna kesho!

– Wakati umefika wa wanaostahili kujitofautisha na wasiostahili, ili kila mtu asiweze kujivunia moyo wa ujasiri!

Nilirudi kwenye mgahawa.

– Je! Umeona kile tulichoumbwa nacho? – mwenye nyumba yangu aliniuliza kwa sifa.

– Hakika nimeona, – Nilijibu, nikiona nguvu yangu imeniacha na kwamba kichwa changu kilikuwa kimejaa hisia za kushangaza.

Siku hiyo hiyo nilisoma kwenye gazeti lao habari iliyoongoza kama hii:

– Wananchi, ni wakati wa kuacha kujivuna bure na kuringa kati yetu; ni wakati wa kuacha kuthamini maneno matupu ambayo tunayotumia kwa maelezo mengi ili kuonyesha tabia zetu za kufikirika na jangwa. Wakati umefika, wananchi, kujaribu maneno yetu na kuonyesha ni nani anayestahili na nani hafai! Lakini tunaamini kwamba hakutakuwa na waoga wa aibu kati yetu ambao watalazimika kuletwa kwa nguvu mahali pa kuweka chapa. Kila mmoja wetu ambaye anasikia katika mishipa yake kuwa damu tukufu ya babu zetu atapambana kuwa miongoni mwa wa kwanza kubeba uchungu na kuteseka, fahari na ukimya, kwa maana huu ni uchungu mtakatifu, ni dhabihu kwa faida ya nchi yetu na kwa ustawi wetu sote. Mbele, Wananchi, kwa kuwa kesho ndio siku ya mtihani mtukufu!…

Mmiliki wa nyumba yangu alielekea kulala moja kwa moja baada ya mkutano ili aweze kufika mapema mahali palipoteuliwa kesho yake. Wengi walikuwa, hata hivyo, walienda moja kwa moja kwenye Ukumbi wa Mji ili kuwa karibu iwezekanavyo kwa mwanzo wa foleni.

Siku iliyofuata pia nilienda kwenye Ukumbi wa Mji. Kila mtu alikuwepo – wachanga kwa wazee, wake kwa waume. Baadhi ya akina mama walileta watoto wao mikononi mwao ili wapewe chapa ya utumwa, hiyo ni kusema kwa heshima, na hivyo kupata haki kubwa ya nafasi za juu katika utumishi wa umma.

Kulikuwa na kusukumana na kuapa (kwa hili walikua kama sisi Waserbia, na nilifurahi kwa hilo), na kila mtu alijitahidi kuwa wa kwanza mlangoni. Wengine walikuwa wakiwakamata wengine kooni.

Chapa zilitolewa na mtumishi maalum wa umma katika suti yake rasmi na nyeupe, ambaye alikuwa akiwakemea watu kwa upole:

– Msinong’one, Mungu wangu, zamu ya kila mtu itafika – nyie sio wanyama, nadhani tunaweza kusimamia bila kusukumana.

Kupata chapa kukaanza. Mmoja akapiga kelele, mwingine alikuwa anaugua tu, lakini hakuna mtu aliyeweza kuvumilia bila kutoa sauti muda wote niliokua pale.

Sikuweza kuvumilia kutazama mateso haya kwa muda mrefu, kwa hivyo nilirudi kwenye mgahawa, lakini baadhi yao walikuwa wamekwishafika pale, kunywa na kunywa.

– Hiyo imekwisha! – alisema mmoja wao.

– Kweli, hatukupiga kelele sana, lakini Talb alikuwa akilia kama punda!… – Alisema mwingine.

– Unaona jinsi Talb wako alivyo, na ulitaka awe kama mwenyekiti wa mkutano jana.

– Ah, kamwe hauwezi kujua!

Waliongea, wakiugua maumivu na uchungu, lakini wakijaribu kuificha, kwani kila mmoja alikuwa na aibu ya kufikiriwa kuwa mwoga.

Kleard alijidhalilisha mwenyewe, kwa sababu aliugulia, na mtu mmoja anayeitwa Lear alikuwa shujaa kwa sababu aliomba kupata chapa mbili kwenye paji la uso wake na kamwe hakutoa sauti ya maumivu. Jiji lote lilikuwa likiongea tu kwa heshima kubwa juu yake.

Watu wengine walikimbia, lakini walidharauliwa na kila mtu.

Baada ya siku chache yule aliye na chapa mbili kwenye paji lake la uso alitembea na kichwa kikiwa juu kwa hadhi, heshima na kujistahi, amejawa utukufu na kiburi, na kila aendapo, kila mtu alimwinamia na kumvulia kofia yake kumsalimia shujaa wa siku hiyo .

Wanaume, wanawake, na watoto walimfuata barabarani ili kuona mtu shupavu zaidi wa taifa hilo. Popote alipoenda, minong’ono iliongozwa na mshangao ulimfuata: ‘Lear, Lear!… Ni yeye!… Huyo ndiye shujaa ambaye hakulia, ambaye hakutoa sauti wakati chapa mbili zilivutiwa kwenye paji la uso wake!’ Alikuwa kwenye vichwa vya habari vya magazeti, akisifiwa na kutukuzwa.

Na alikuwa anastahili kupendwa na watu.

Katika mahali pote ninasikiliza sifa kama hizi, na ninaanza kuhisi damu tukufu ya zamani ya Serbia ikitembea kwenye mishipa yangu, babu zetu walikuwa mashujaa, walikufa walemavu kwenye vijiti kwa uhuru; sisi pia tunao ushujaa wetu wa zamani na Kosovo yetu. Ninafurahi na kujivunia kwa ubatili wa kitaifa, nina shauku ya kuonyesha jinsi uzao wangu ulivyo jasiri na kukimbilia Ukumbini na kupiga kelele:

– Kwa nini mnamsifu Lear wenu?… Hamjawahi kuona shujaa wa kweli! Njooni mjionee wenyewe damu tukufu ya Serbia ilivyo! Weka chata kichwani mwangu, sio mbili tu!

Mtumishi wa umma katika suti nyeupe alileta chapa yake karibu na paji langu la uso, na nikaanza… Niliamka kutoka kwenye ndoto yangu.

Nililisugua paji langu la uso kwa hofu na nikajiwazia, nikishangaa vitu vya kushangaza ambavyo vinaonekana katika ndoto zangu.

– Karibu ningefunika utukufu wa Lear wao, – Nikawaza na, kuridhika, nikageuka, na nilisikitika kidogo kwa sababu ndoto yangu haikukamilika.

 

Huko Belgrade, 1899
Kwa mradi wa “Radoje Domanovic” uliotafsiriwa na John N. Lusingu, 2020